Friday, July 26, 2013

MAREKANI KUCHELEWESHA NDEGE KWA MISRI



MAREKANI imesema kuwa itachelewesha mpango wake wa kuikabidhi Misri ndege za kivita aina ya F-16 huku mgogoro wa kisiasa ukiendelea kutokota nchini Misri kufuatia kuondolewa mamlakani kwa aliyekuwa Rais Mohammed Morsi.
Msemaji wa idara ya ulinzi nchini Marekani, George Little alisema kuwa uamuzi huo ulifikiwa kutokana na hali inayokabili Misri kwa sasa.
Marekani inadadisi ikiwa kuondolewa mamlakani kwa Morsi ilikuwa mapinduzi ya kijeshi, hali inayoweza kusababisha Marekani kusitisha msaada wake kwa Misri. (HM)
Hapo jana mkuu wa jeshi la Misri Generali Sisi , aliitisha maandamano ya umma akiwataka wananchi kuliruhusu jeshi kukabiliana na kile alichokiita tisho la ugaidi.
Lakini Abdel Fattah al-Sisi aliongeza kuwa hakuwa anaitisha maandamano kwa lengo la vurugu huku akiwasihi wananchi kuwa na maridhiano.
Katika jibu lake kwa wito wa jeshi, chama cha Muslim Brotherhood, ambacho kinamuunga mkono Morsi, kilisema kuwa Generali Sisi alikuwa anaitisha vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Ndege hizo nne aina ya F-16 ni sehemu ya ndege nyingine 20 ambazo zimeitishwa, kati ya hizo nane tayari zikiwa zimepelekwa Misri.
Hata hivyo Marekani iliahidi tarehe 11 mwezi Julai kuwa bado ina mpango wa kuikabidhi Misri ndege hizo. Chanzo: bbcswahili

No comments:

Post a Comment